Navigation Menu

Moshi Diocese at P.O. Box 3011, Moshi, Kilimanjaro n/a TZ - Mwondoko wa Awamu Mpya - MH. ASKOFU  AMANI 

Mwondoko wa Awamu Mpya - MH. ASKOFU  AMANI 

               MWONDOKO  WA  AWAMU  MPYA

 Utangulizi.

 

Kwa vile jimbo letu limeshaadhimisha miaka 100 ya imani, tunamshukuru Mungu kwa urithi wa Injili na maendeleo yote waliotuletea Wamisionari.  Wazee wetu walipokea imani, wakaifanyia kazi na sasa ni zamu yetu tuiendeleze na tukolee zaidi katika tamaduni za kikristo.  Ulimwengu wa leo unahitaji ushuhuda wa dhati kutoka kwetu sisi tunaotegemewa kuwa chumvi na mwanga katika sekta zote za maisha.  Utambulisho wetu hasa ni kuwa chumvi ya dunia na mwanga wa ulimwengu.  Je! Uwepo wetu katika jamii huleta matumaini kwa watu na utukufu kwa Mungu? (Mt. 5:13-16).Kweli ukristo ni changamoto kubwa.

Tutumie tuliyo nayo hasa taasisi zetu kama familia, JNNK, Mashirika ya kitume, ziwe mahali pa kuimarishia imani, utu bora na mshikamano utakaojionesha katika maisha ya sala na fadhila za kikristo.  Juhudi mbalimbali zitumike ili waamini wasome na kuielewa Biblia iliyo habari njema kutoka kwa Mungu kwamba sisi ni wanawe na tupangilie maisha iwapasavyo watoto wa Mungu.  Waamini wote waone fahari kulishwa na Mungu kwa njia ya Ekaristi itupayo nguvu tuweze kuwajibika kwa imani, matumaini na mapendo. 

Sisi sote tumkiri Kristo kuwa Bwana na Mkombozi wetu na kuachana na desturi za kutafuta usalama kwa mizimu,  waganga wa ramli na wapiga bao yaani fikra na matendo ya kishirikina.  Hali kadhalika, fikra za kibaguzi na dharau kati ya watumishi wa Mungu sio za  kimungu bali za yule mwovu kwa uhakika.  Mila, tamaa, desturi na mazoea yanayopingana na maagano ya ubatizo ni fedheha tupu kwa mfuasi wa Yesu.. Ibilisi akiotesha ndago hutumia vibarua wake kuzipalizi.  Mtume Pauli anatuasa:  “Basi, acheni mwenendo wenu wa awali, yaani ule utu wenu wa kale uliokuwa unaangamizwa kwa tamaa zake danganyifu.  Jirekebisheni upya rohoni na katika fikra zenu.  Vaeni hali mpya ya utu ambayo imeumbwa kwa mfano wa Mungu na ambayo hujionesha katika maisha ya kweli ya uadilifu na utakatifu” Ef.4: 22-24.  Basi, sisi sote twatakiwa tuishi maisha ya shukrani kwa kushika amri za Mungu na kushika kiaminifu viapo vyetu vya Ubatizo, Komunyo ya kwanza, Kipaimara, Ndoa, Nadhiri na Daraja.

 

Hiyo ndiyo njia itakayotuwezesha kupokea mwanga wa Kristo na jimbo letu litakuwa na baraka za miito yote kwa wingi. Hayo ndiyo matumaini yangu wakati tunapoanza awamu ya kipindi kipya jimboni.  Kwa njia ya kuwajibika na kushirikiana katika Kristo tutafikia umoja tulioombewa na Kristo kwenye sala yake maalum kwa wafuasi wa nyakati zote.(Yoh. 17).  Kwa sasa, wafuasi ni sisi, wewe na mimi; kila mwamini katika kazi na nafasi yake kwenye jamii.  Tuombe mwanga wa Roho Mtakatifu wa kuona na kuoneshana njia itupasayo kupita, na ujasiri wa kushirikiana katika kuyakabili matatizo na pingamizi za maisha kwa matumaini tukiyazingatia maneno ya  mtume Paulo kuhusu upendo wa Mungu kwetu:  “Tumepata ushindi mkubwa kwa msaada wake yeye aliyetupenda.  Maana ninajua hakika kwamba hakuna kitu kiwezacho kututenganisha na upendo wake: wala kifo, wala uhai; wala malaika au nguvu nyingine za mbinguni; wala yanayotokea sasa, wala yatakayotokea baadaye; wala mamlaka; wala ulimwengu wa juu, wala wa chini kabisa.  Hakuna kiumbe chochote kitakachoweza kututenga na upendo wa Mungu katika Kristo Yesu Bwana wetu” Rom.8:37b-39.

 

NEMBO

Sikukuu  ya Ukulu wa Mt. Petro Mtume hufanyika tarehe 22 Februari.  Sikukuu hii imeadhimishwa Roma tangu karne ya  nne.  Hii ni alama ya umoja wa  Kanisa lililojengwa na Kristo juu ya mwamba mtume  Petro. Mt.16: 18 – 19.   Ni siku maalum ya kuomba  mshikamano na ustawi wa Kanisa jimboni na ulimwenguni kote.  Maklero, watawa na walei kwa pamoja washirikiane kutekeleza majukumu yawapasayo kama watu wa Mungu.

Nimeichagua tarehe hii iwe siku ya kuwekwa kwangu wakfu kwa sababu hitaji letu kubwa hapa Jimboni Moshi ni mshikamano utakaotokana na kuwajibika na kushirikiana katika Kristo. Kanisa haliwezi kuwa hai na la mafanikio wanakanisa wasipowajibika na kuchangia nguvu kwa pamoja.  Ninaamini tunaweza kufikia malengo ya kiinjili endapo tutayafanyia kazi kwa pamoja.

Baada ya uteuzi kutangazwa, askofu mteule aliambiwa aandae NEMBO.

Nembo hukusudiwa ioneshe TASWIRA ya uchungaji.  Kaulimbiu ninayoweka mbele yangu ni:  “KUWAJIBIKA NA KUSHIRIKIANA KATIKA KRISTO”.

Tunapoanza awamu mpya ya Jimbo letu, natafakari jimbo ambalo limeshaadhimisha miaka 100 ya kupokea imani ya kikristo.  Tumefikia hatua ya kufurahia matunda ya miaka karibu 120 ya imani na kuimarisha tuliyo nayo kwa ajili ya vizazi vijavyo.  Namna yetu ya kuishi imani kiinjili inatuwajibisha tumtazame na tujiunge kwa umakini zaidi na Mkombozi wetu. Yeye ametuita kutoka gizani  na kutuweka katika mwanga wa maisha mapya ya neema. Mtume Petro anaeleza vizuri anaposema:  “Kwa uwezo wake wa kimungu, Mungu ametujalia mambo yote tunayohitaji ili tuishi maisha ya kumcha Mungu kwa kumjua yeye aliyetuita tuushiriki utukufu na wema wake yeye mwenyewe.” 2Pet. 1:3.

                               

 TULIKOTOKA

Wamisionari watatu wa Shirika la Roho Mtakatifu walifika Kilimanjaro kwa mara ya kwanza tarehe 15 Agosti 1890 wakiongozwa na Askofu wa Vikarieti ya Zanzibari Mhashamu Jean Marie Raoul de Courmont.  Wengine walikuwa mapadre Auguste Commenginger na Alexander Le Roy pamoja na wapagazi Nderingo na wenzake wachache.  Ujio huo ulifungua Kilimanjaro kwa utume wa kijasiri wa wamisionari kwa muda wa miaka 20.

 

Juhudi kubwa za kusimika Injili katika eneo hili zilizaa matunda pale Papa Pius X alipoafiki ombi la kuwepo kwa Vikarieti ya Kilimanjaro.  Alimteua Askofu Maria Joseph Aloyse Munsch kuwa mtawala wake kuanzia tarehe 13 Septemba 1910.  Eneo husika ni majimbo tunayofahamu leo kuwa Tanga, Same, Moshi, Arusha, Mbulu na sehemu ya jimbo la Dodoma.  Wakati huo wamisionari walishaweka vituo vya misioni Kilema 1890, Kibosho 1893, Rombo Mkuu1896, Tanga, Mlingano, Gare, Irente, Ufiomi, Kondoa Irangi, Kilomeni na Galapo.  Jumla ya wakristo ilikuwa 4,000 na wakatekumeni 8,000.  Mapadre wamisionari 18, Mabradha 12 na Masista 26 wa Shirika la Damu Takatifu.  Masista hawa walifundisha katekisimu na masomo mengine shuleni, walitunza wagonjwa na yatima, walifundisha akina mama maarifa ya nyumbani na waliwapatia mapadre huduma za kimaisha kama usafi na chakula.  Waliendelea kutoa huduma hizo mpaka Masista wazawa walipoweza kumudu majukumu hayo kwa ajili ya utumishi wa Mungu.  Tangu mwanzo wa kufika kwao Kilimanjaro, wamisionari walifanya Kilema kuwa kituo na makazi yao makuu.  Ndiyo maana Askofu Munsch alichagua Kilema kuwa mahali pa kupangia taratibu za utawala na uchungaji wa Vikarieti mpya.  Maisha ya imani ya kikristo Kilema yalichochewa na uwepo wa wamisionari katika eneo hilo na pia juhudi kubwa ya makatekista walioandaliwa  na mapadre ili kusaidia utume wa kueneza Injili.  Kauli mbiu ya Askofu Munsch ilikuwa: “NON EGO SOLUS SED GRATIA DEI MECUM” (SIYO MIMI BALI NEEMA YA MUNGU).  Kwa imani na ujasiri  Askofu Munsch na wasaidizi wake  waliimarisha vituo vya misioni mpaka vita vya kwanza vilipoanza 1914.  Wakati wa vita baadhi ya vituo vilishambuliwa na vingine vikafungwa.  Wamisionari wajerumani walilazimishwa kujiunga na jeshi la Ujerumani.  Askofu Munsch aliwekwa kizuizini Tanga kwa muda kasha akarudishwa Ulaya mwaka 1918.  Wakati wa vurugu za vita  Padre Auguste Commenginger alisimamia Vikarieti (1918-1922).  Kwa ujumla wakristo walibaki imara katika imani wakisaidiwa na makatekista.  Baada ya Ujerumani kushindwa vita, utawala ulichukuliwa na Uingereza na ikabidi waletwe wamisionari wenye kuzungumza kiingereza

 

Askofu Henry Aloyse Gogarty alisimamia Vikarieti 1922-1924 na kuwa Mtawala wake 1924-1931.  Mhashamu Gogarty aliona umuhimu wa kuandaa Wainjilishaji wazawa ili wapeleke Injili mbele.  Kauli mbiu yake ilikuwa: “O ORIENS VENI ET ILLUMINA” (NYOTA YA MASHARIKI NJOO UANGAZE).  Aliamini kwamba Elimu na malezi vingeleta mwanga katika maisha ya Kanisa changa.    Alifungua seminari ya Mt.  Yakobo Kilema Chini mwaka 1925 kwa ajili ya kuandaa mapadre wa vikarieti ya Kilimanjaro na hata Kenya.  Mwaka 1926 alifungua kituo Singa Chini kwa ajili ya kuwaandaa Walimu, Makatekista na mafundi wa fani mbalimbali.  Kituo kilivuma kwa kuandaa walimu bora na viongozi mahiri wa jamii.  Shule za wasichana zilifunguliwa Kilema na Kibosho kuwaandaa walimu wanawake.  Mwaka 1931 alianzisha Shirika la Masista wa Bibi yetu wa Kilimanjaro huko Huruma Rombo.  Askofu Gogarty aliweka taratibu na kanuni msingi za mashirika ya kitume ya walei kama tunavyoyaona leo.  Kweli, aliweka misingi ya malezi na vituo vya misioni vikawa vivutio na vichocheo vya maendeleo ya imani na jamii.  Mafanikio makubwa yalipatikana baadaye ambayo yalidhihirishwa kwa idadi nzuri ya maklero wazawa wenye ari ya uchungaji, watawa wachapa kazi na idadi ya waamini wasomi waliokuwa wakereketwa wa imani.

 

Askofu Joseph Byrne alitawala Vikarieti Kilimanjaro (1933-19530 na Jimbo Moshi (1953-1959).  Kauli mbiu yake ilikuwa: “SUB TUUM PRAESIDIUM” (TUNAUKIMBILIA ULINZI WAKO).  Alikuwa na heshima kubwa sana kwa Mama Bikira Maria.  Mhashamu Byrne alipokea Vikarieti iliyokuwa na vituo vya kuwaandaa walezi kama ilivyoelezwa hapo juu.  Idadi ya wakristo ilikaribia 31,000.  Kwa miaka 20 ya kwanza aliendeleza na kuboresha mipango ya watangulizi wake.  Alienzi sana elimu, afya na imani Katoliki.  Aliwahimiza wazazi wapeleke watoto shule ili wapewe elimu.  Alikazia maisha ya utakatifu na elimu kwa waamini wa nyanja zote.  Askofu Byrne alitambua umuhimu wa Shirika la watawa wa kiume katika vikarieti.  Hivyo basi, Shirika la Mabradha wa Moyo Safi  wa Maria lilianza tarehe 2-2-1947 huko Maua chini ya malezi ya Shirika la Roho Mtakatifu. Wanachama walijiunga kutoka maeneo mbalimbali ya vikarieti.  Mabradha walisaidia sana kusimamia shughuli za ujenzi wa makanisa,shule,hospitali; kilimo na uendeshaji wa shule za ufundi wa fani mbalimbali. Vikarieti ilikua kiimani na kiidadi hata  Roma ikakubalia marekebisho ya mipaka ili kurahisisha usimamizi.

Dodoma iliwekwa katika uangalizi wa Shirika la Pasionisti (4-1-1935).

Mbulu ilikabidhiwa kwa Wapalotini (13-3-1943).

Tanga ilifanywa ‘Prefecture’ na kukabidhiwa kwa Shirika la Rosminiani(18-4-1950).

Moshi ilifanywa kuwa Jimbo tarehe 25-5-1953 na Askofu wa kwanza alikuwa Mhashamu Joseph Byrne.  Alitawala kwa miaka 6 eneo la Same, Moshi na Arusha.  Tunahesabu utawala huu kama awamu ya kwanza kumaanisha askofu wa kwanza wa Jimbo.  Mwaka 1959 Askofu Byrne alistaafu akiacha waamini 140,000, zaidi ya mapadre wazawa 20 na zaidi ya masista wazawa 130.  Parokia 16 zilizinduliwa wakati wake na nyingi zilipewa majina ya kumpa heshima Mama wa Mungu..  Hayo yalikuwa matokeo ya kazi ya Mungu iliyofanyika siku nyingi na kwa njia ya watu wengi.

 

Awamu ya pili ilimwangukia Padre mzawa na pia mtawa wa Shirika la Roho Mtakatifu aliyepewa uaskofu na Papa Yohani XXIII tarehe 8-5-1960, Mhashamu Joseph Kilasara.  Kauli mbiu yake ilikuwa: “PER MARE ET PER TERRAS” (KATIKA BAHARI NA NCHI KAVU).  Hayo yalikuwa matashi ya kueneza utawala wa Mungu kila mahali.  Baada ya kupewa uaskofu aliagizwa kuhamisha makao kutoka Kilema na kuyaweka katika mji mkubwa wa jimbo.  Alifanya hivyo kwa kuhamishia makazi na ofisi katika parokia ya St. Louis Moshi ambayo ilipewa hadhi ya kuwa Kanisa Kuu na jina jipya Kristo Mfalme.  Alihimiza ujenzi wa Kanisa Kuu la sasa na kuzindua maparokia 7 wakati wa utawala wake.  Askofu Kilasara alitengeneza miundo mbinu za afya na elimu jimboni.  Alihamasisha ufunguzi wa Kilimanjaro Boys’ na Kibosho Girls’ kwa ajili ya kuandaa viongozi bora.  Alishughulikia  ujenzi wa Community Centre na upatikanaji wa nyumba anakoishi Askofu sasa.  Kwa ushauri wake kwa wahusika,  mipaka ya jimbo iliendelea kurekebishwa:  Arusha ilifanywa kuwa jimbo 1-3-1963 na Same ikawa ‘Prefecture’ 10-12-1963 na hatimaye 1979 ikawa jimbo la kujitegemea.  Mchango wa Askofu Kilasara ni wa kihistoria kwa vile aliliingiza jimbo katika vuguvugu la nchi kupata uhuru.  Raia wengine hawakuelewa kwamba bila kuwajibika uhuru ungebaki ni wa bendera tu!  Heshima ya mwanadamu ni kufanya kazi na kujitegemeza.  Askofu alihimiza kwa mafundisho na matendo azma ya serikali kupiga vita maadui wakuu watatu, yaani ujinga, maradhi na umaskini.    Kutokana na sababu za kiafya alijiuzulu mwaka 1966 na alipofariki Novemba 1978, alizikwa  katika  kanisa la Kilema iliyokuwa Kanisa Kuu la kwanza la Jimbo.

 

Awamu ya tatu:  Monsinyori Joseph A. Sipendi aliyekuwa mtawala wa jimbo la Kipapa Zanzibar aliteuliwa kuwa Askofu wa Jimbo la Moshi.  Alipewa daraja la Uaskofu tarehe 24-3-1968 katika Kanisa Kuu la Kristo Mfalme.  Aliona hitaji kubwa na muhimu ni kuwasaidia watu wamjue Mungu, wampende na kumtumikie.  Aliendeleza kazi zilizokuwa zimeanzishwa na mtangulizi wake katika nyanja za uchungaji, uinjilishaji na maendeleo ya jamii akikazia hasa elimu na afya.  Alianzisha miundo mbinu ya kulitegemeza jimbo kama vile mradi wa shamba la Kilacha, nyumba ya kupangisha hapa mjini, na kuhimiza mapadre na waamini walenge kulifanya kanisa mahalia lijitegemee kiutumishi na kiutawala (uongozi), kiuinjilishaji na kiuchumi.  Alisifia ubunifu na kupiga vita uvivu. 

Aliona Kanisa linao wajibu wa kuwasaidia watu waishi kama binadamu katika kupata mahitaji yao ya lazima ya roho na ya mwili na pia kuishi kindugu kama watoto wa Mungu na taifa teule.  Kwa hiyo aliimarisha huduma za afya kwa kuendeleza hospitali za Huruma, Kilema na Kibosho.  Kwa upande wa elimu alihimiza kuanzishwa shule za sekondari za wazazi zikiongozwa na Kanisa hususan Jimbo.  Askofu Sipendi alishughulikia malezi ya waseminaristi na mapadre kwa lengo la kuwapata wahudumu bora wa Kanisa ambao wangewahubiria watu Injili, kuwafafanulia  mafundisho ya Kanisa kwa usahihi, kutoa ushuhuda wa mapendo ya Yesu kwa mtindo wa maisha yao.  Aliwaona walezi kama mawakala wa mapinduzi ya kweli ya maisha ya binadamu mkristo.  Aliwataka watu wafanye kazi, washirikiane, na wajenge undugu wa upendo.  Aliwataka mapadre na watawa waishi Injili kwa matendo kuliko kuhubiri kwa maneno matupu.  Aliwaalika waamini wote waithamini na kuishi Injili waweze kuwa kweli taifa jipya la Mungu.  Kauli mbiu yake  KWA JINA LA YESU ilikuwa ndiyo msukumo wa juhudi zake za kuinjilisha, kutawala na kujenga kanisa hai jimboni Moshi.  Ndiyo maana aliimarisha baraza la Walei na WAWATA, ujenzi na uimarishaji wa JNNK, upanuzi wa huduma za kijamii, upanuzi wa seminari ndogo Kilema na kubwa Kibosho, na kuwapeleka mapadre na watawa kwa masomo ya juu.  Katika kipindi hiki parokia 10 zilifunguliwa, mashirika mapya manne ya kitawa yalikaribishwa jimboni.  Askofu Sipendi aliugua kwa muda, akaaga dunia tarehe 23-4-1985 na kuzikwa katika Kanisa Kuu la Kristo Mfalme tarehe 27-4-1985.

 

Awamu ya nne:  Kwa takribani kipindi cha mwaka moja, jimbo liliongozwa na Mtawala Jimbo Msgr. Arbogast Sekundo.  Awamu hii ilimwangukia aliyekuwa Padre Mlesi wa miito jimboni, Mhashamu Amedeus P. Msarikie.  Alipewa daraja la Uaskofu tarehe 1-5-1986 na Mwadhama Josef Kardinali Tomko kutoka Vatikano wakati wa mkutano Mkuu wa AMECEA uliokuwa unafanyika mjini Moshi.

Askofu Msarikie aliieleza azma yake katika kaulimbiu:UMOJA KATIKA UPENDO, yaani mshikamano wa kijimbo. Alihimiza uimarishaji wa uchungaji kwa kuboresha malezi ya waseminaristi, watawa na mapadre.  Aliendeleza uboreshaji wa huduma za afya na elimu jimboni pote.  Alihimiza ujenzi bora wa makanisa, nyumba za mapadre, konventi za watawa na utunzaji wa mazingira.  Aliimarisha ofisi kuu ya Jimbo na idara zake kwa ajili ya kuboresha huduma za kichungaji hapa jimboni na hata kushiriki ngazi za kanda na kitaifa.  Shirika la Mabradha wa Jimbo lilifanyiwa marekebisho na kupewa jina Mabradha wa Yesu Mkombozi na makao yao yakawa  Kilacha Himo.

Kwa kuzingatia alama za nyakati hususan kuboresha elimu, Askofu Msarikie ameanzisha Chuo Kikuu cha Mwenge MWUCE kwa lengo la kuandaa walimu bora wa kufundisha shule za Sekondari za jimbo na Seminari.  Amejenga kituo cha Moyo Mt. wa Yesu Longuo kwa ajili ya kuwa na nyumbani kwa mapadre na kituo cha malezi endelevu.  Amejenga kituo cha ufundi Karanga kuwasaidia vijana kujiandaa kwa utumishi wa jamii.              Askofu Msarikie alifanikisha mengi jimboni na taifani.  Wakati wa awamu yake alikazana kuimarisha umoja na mshikamano wa kijimbo pia alihimiza ufundishaji dini shuleni na vyuoni.  Mara nyingi alihimiza uchungaji sahihi na makini kama ule wa Yesu Mchungaji mwema.  Hali kadhalika aliagiza umakini katika maadhimisho ya kufaa ya liturjia na ibada nyingine.

Mhashamu alisimamia vyema matayarisho  na maadhimisho ya Yubilei ya miaka 100 ya Ukatoliki Moshi na kumkaribisha hayati Papa Yohane Paulo II hapa Moshi Septemba 4-5,1990.

Alihimiza pia matayarisho na adhimisho la Yubilei ya Ukombozi mwaka 2000 iliyofanywa  kiulimwengu.  Ama kweli awamu hii ilikuwa na matukio makubwa ya kusherehekea.  Mwaka 2003 Jimbo liliadhimisha Yubilei ya Dhahabu (miaka50).  Tunapotafakari mwaka huu wa JNNK tunazidi kutiwa moyo na msisitizo wa Askofu Msarikie wa malezi endelevu ya Halmashauri Walei na vyama na mashirika ya kitume ili watu wote wa Mungu wazidi kukomaa katika kumjua Mungu na  kumpenda yeye na jirani.

Askofu Msarikie ametumia muda na nguvu zake nyingi na sadaka mbalimbali katika utume wake jimboni na taifani.  Amekuwa mkarimu kwa kushirikisha vipaji vyake akaliongoza na kuliendeleza jimbo la Moshi kwa miaka 21 mpaka alipostaafu akiwa na afya na nguvu tele na kukabidhi jimbo kwa askofu wa awamu ya tano, ndiyo awamu mpya inayoelezwa hapa.  Tunapotafakari historia ya jimbo letu tujione katika mpango Mwenyezi Mungu aliofichua kwetu.  Kwanza ni kumshukuru Mungu kwa makuu aliyotutendea kama wanajimbo.  Tunawiwa mengi na watangulizi wamisionari na walimu wote wa dini waliojitoa kuinjilisha katika mazingira magumu.   

 

Tunapenda basi nembo  husika ioneshe ni kwa namna gani tutapokea Injili, kuifanyia kazi  na kufurahia matunda yake. Paulo mtume anatuuliza Wamoshi: “Je, maisha yenu katika Kristo yanawapeni nguvu?  Je, mapendo yake yanawafarijini?  Je, mnao umoja na Roho Mtakatifu na kuoneana huruma na kusikitikiana ninyi kwa ninyi?  Basi, ikamilisheni furaha yangu kwa kuwa na fikra moja, upendo mmoja, moyo mmoja na nia moja.” Fil. 2: 1-3.  Jibu letu liweje?  Tupitie alama katika nembo:  Nembo itakuwa na alama 7:  Msalaba, Biblia, Ekaristi, Nyota, Mlima Kilimanjaro, Tambarare ya kijani  na Kauli mbiu yenyewe.

1.Msalaba:  Tumekombolewa kwa upendo wa ajabu kwa njia ya msalaba wa Mkombozi wetu na twatakiwa tufahamike kuwa wafuasi hai :  Kama mtu yeyote anataka kuwa mfuasi wangu, lazima ajikane mwenyewe, auchukue msalaba wake, anifuate.” Mk. 8: 34. Tuone fahari katika msalaba, tusiuonee aibu wala kuuaibisha kwani ukombozi wetu umepatikana hapo: “Maana kwa njia ya msalaba huo ulimwengu umesulubiwa kwangu, nami nimesulubiwa kwa ulimwengu” Gal. 6:14b. Twajibariki kwa ishara ya msalaba tukitamka majina matakatifu ya Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Twabatiza na kubariki kwa Utatu Mtakatifu. Mungu wetu ni UMOJA; tuutafute umoja. Kwa hiyo msalaba utukumbushe wajibu wetu wa kubeba misalaba yetu na pia kuwasaidia wengine  kuichukua misalaba yao (Gal. 6: 2, 5).

 

2.Biblia:  Mungu husema nasi kwa njia ya Maandiko Matakatifu.  Yesu anatuambia: “Kama mkiyazingatia mafundisho yangu mtakuwa kweli  wanafunzi wangu.  Mtajua ukweli, nao ukweli utawapeni uhuru” Yoh. 8:31-32. Mungu wetu hutulea kwa kuja kwetu na kubisha mlango wa nafsi zetu. Kuna mawili:  Kumpokea au kumkataa!  “Heri zaidi wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika.” Lk. 11: 28. “Mtu akisikia sauti yangu  na kufungua mlango, nitaingia nyumbani kwake na kula chakula pamoja naye, naye atakula  pamoja nami.” Asema Yesu Ufu. 3: 20.  Kweli neno la Mungu “ni taa ya kuniongoza, na mwanga katika njia yangu” Zab. 119:105.  Ni wajibu wetu kulipenda, kulisoma na kulitafakari neno la Mungu ili tupate mafundisho ya Mungu yenye kutupatia maisha ya neema na utakatifu; ndiyo njano izungukayo Biblia katika nembo yaani kuangaziwa na mafundisho ya Mungu tuishi uadilifu, wema, na kuwa watu wa  sala kama Mwalimu wetu Yesu.

 

3.Ekaristi:”Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu, akaa ndani yangu, nami nakaa ndani yake”Yoh. 6:56.  Hatuna njia bora ya kushikamana na Mungu wetu kuliko kuungana na Mwanaye katika sakramenti ya Ekaristi. Huu ni mkate hai ulio tofauti na lishe nyingine zote. Yesu mwenyewe anasema: “Mimi ni mkate hai ulioshuka  kutoka mbinguni.  Mtu yeyote akila mkate huu ataishi milele.  Na mkate nitakaompa  ni mwili wangu ninaoutoa kwa ajili ya uhai wa ulimwengu” Yoh. 6:51. Kwenye nembo  Ekaristi imezungukwa na rangi ya zambarao kuonesha kwamba yatupasa tujitakase kwa toba kabla ya kushiriki meza ya Bwana tusije tukajiingiza hukumuni kwa njia ya mwili na damu ya Bwana 1Kor.11:27. Tena “Jitakaseni, mkatupe mbali chachu ya kale ili mpate kuwa donge jipya lisilotiwa chachu kama mnavyopaswa kuwa; maana, Kristo, Pasaka yetu, amekwisha tolewa  kuwa sadaka. Basi, tufanye karamu hiyo si kwa chachu ile ya kale, chachu ya ubaya na uovu, bali kwa mkate usiotiwa chachu, mkate wa usafi na kweli” 1Kor. 5: 7-8.  Katika Ekaristi twaonja upendo, msamaha, ukomavu wa utu, mwungano na uhakika wa maisha mapya ya kushiriki hali ya kimungu.  Katika Ekaristi twachota nguvu zote tunazohitaji za kupambana na maadui shetani, ubinafsi na malimwengu.  Katika Ekaristi twaponywa maradhi ya roho,mwili na mahusiano na kukaribishwa kuanza maisha upya kwa matumaini. Yesu atualika tumpelekee yaliyotusonga akituahidia faraja na kitulizo kamilifu  cha kimungu (Mt. 11:27-30). Ama kweli Ekaristi ni kitovu cha maisha ya mkristo. Kwa hiyo tuipende sana Ekaristi, tuithamini na kuitunza dhidi ya kufuru zo zote za binafsi au za jamii.

 

4.Nyota: Nyota iliwaongoza Mamajusi mpaka mahali alipozaliwa Mwokozi.  Mwokozi wetu anatuambia: “Mimi ndimi mwanga wa ulimwengu.  Anayenifuata mimi hatembei kamwe gizani, bali atakuwa na mwanga wa uhai.Yoh. 8:12.  Tuwe na imani thabiti na Mkombozi wetu.  Hakuna mwingine wa kutegemewa isipokuwa huyo aliyetimiza kikamilifu mpango wa Baba wa kutufanya huru: “Nami nitakapoinuliwa juu ya nchi nitamvuta kila mmoja kwangu” Yoh. 12:32 . Hakika “Mwanakondoo aliyechinjwa anastahili kupokea uwezo, utajiri, hekima, nguvu, utukufu na sifa”Ufu. 5: 12. Maisha na mafundisho ya Yesu ni lugha ya Mungu wetu  ya kutuonesha  ukamilifu wa upendo wake kwetu sisi viumbe vyake. Tuifuate nyota hiyo ili tuishi maisha ya faida na pia kuwa na fikra za kimungu kama tunavyoelekezwa katika Injili.  Kristo mwanga wetu atuangaze na kutuongoza kila mtu binafsi na katika taasisi zetu zote hapa jimboni, taifani na ulimwenguni kote. Kwa nguvu ya Msalaba, kwa mafundisho ya Biblia na kwa mwungano wa Ekaristi tuna hakika na misha yetu ya imani kwa  Yesu  Bwana na Mkombozi wetu.. Waliokombolewa huwa na mawazo yaliyokombolewa, mitazamo iliyo sahihi, na tabia za kufaa: “Msiige mitindo ya ulimwengu huu, bali Mungu afanye mabadiliko ndani yenu kwa kuzigeuza fikira zenu.  Hapo ndipo mtakapoweza kuyajua mapenzi ya Mungu na kutambua jambo lililo jema, linalompendeza na kamilifu” Rom. 12:2.

 

5.Mlima Kilimanjaro:  Kibo na Mawenzi:  Hili ndilo jimbo letu.  Mungu mwenyezi ametupa mahali bora na pazuri pa kuishi.  Watu wengi duniani wanatamani wangeishi mahali hapa. Makundi kwa makundi huja kutalii na kushuhudia utukufu wa Mungu ulio katika hifadhi ya Kilimanjaro.”Mungu alipoumba kazi zake mwanzoni, alizifanya ziwepo na kuzipa mpango, akazipa mpango wa kufuata milele, tangu mwanzo wake na vizazi vyote” Sira 16: 26-27a.  Mungu aliiumba dunia, akaifanya imara ili ikaliwe na watu. Isa. 45: 18

Yatupasa kutunza mazingira tuliyopewa na Mungu yakiwa ni urithi wa hapa duniani.  Njia bora ya kuthamini urithi ni kuuheshimu, kuutunza na kuuendeleza. Tunapotazama Kibo na Mawenzi tukumbuke fadhili zote za Mungu na tuhimizane kuboresha mazingira tunamoishi.  Kwa mantiki hiyo hiyo tukazane kulitunza na kuliendeleza Kanisa jimboni, taifani na ulimwenguni. Tujenge tabia ya kuthamini na kutunza yaliyopo, na kuyaendeleza kwa kuboresha huduma na maisha. Ni heshima na fahari kutunza mazingira; ni aibu na fedheha kuharibu au kutelekeza urithi tuliopewa na Mungu na vizazi vilivyopita.  Tutaachia kizazi kijacho urithi gani?

 

 

6.Tambarare ya kijani.  Hawa ndio wakazi wa  Kilimanjaro hasa wa jimbo la Moshi.  Watu wote wanaoishi katika eneo hili ndio utajiri wa kwanza wa taifa na kanisa. Kanisa la Moshi kimsingi lina makundi matatu:  Walei, Watawa na Maklero.  Kila kundi lina umuhimu na umaarufu wake katika uhai wa Kanisa.  Mtaguso wa pili wa Vatikano uliainisha vizuri jinsi makundi hayo yanavyopaswa kushirikiana na kutajirishana kwa lengo la kuishi Injili kwa  umakini kwani changamoto za ulimwengu wa leo zadai hivyo.  Rangi ya kijani yaashiria hali ya kuchipua na kusitawi kwa waamini wa ngazi zote.  Hiyo ni changamoto ya kumkaribisha Roho Mtakatifu atuwezeshe kushika nafasi zetu katika mpango wa Mungu ambao ni “kukusanya pamoja  viumbe vyote, kila kitu mbinguni na duniani, chini ya Kristo” Ef. 1: 10.  Tunakusanywa pamoja kwa  ubatizo, imani, msamaha, toba, na kuyafanya marekebisho ya fikra na mawazo ili tuvae hali mpya ya utu “ambayo imeumbwa kwa mfano wa Mungu na ambayo hujionesha katika maisha ya kweli ya uadilifu na utakatifu.  Matashi ya Mtume Paulo kwa Waefeso yawe sala yetu: “Tumwombe Mungu, kadiri ya utajiri wa utukufu wake, atujalie kwa uwezo wa Roho wake, nguvu ya kuwa imara ndani yetu, naye Kristo akae mioyoni mwetu kwa imani.  Tunamwomba tupate kuwa na mzizi na msingi katika mapendo kusudi tuweze kufahamu pamoja na watu wote wa Mungu jinsi upendo wa Kristo ueneavyo kwa mapana na marefu, kwa kimo na kina.  Naam, tupate kujua upendo wa Kristo upitao elimu yote, tujazwe kabisa utimilifu wote wa Mungu” (3:16-19). Mklero, Mtawa na Mlei WAZUNGUMZE bila kuogopana wala kudharauliana jinsi kila mmoja alivyo na uwezo, utayari na wajibu wa kuchangia karama, mawazo na mang’amuzi ya maendeleo.  Zama za kungojea kuambiwa tu na za kutosilkiliza wengine hazina tija, tena zimepitwa na wakati.

                             

                                                  MAISHA  HALISI.

 

a). Mklero anatarajiwa kuwajibika na kushirikiana na watu mbalimbali ili mpangilio wa matumizi ya muda na nguvu zake udhihirishe kwamba aliwekwa wakfu kwa ajili ya kushiriki ukuhani wa Kristo mwenyewe.  “Kila kuhani mkuu ambaye huchaguliwa miongoni mwa watu hupewa jukumu la kushughulikia mambo ya Mungu kwa niaba ya watu, kutolea zawadi na dhabihu kwa ajili ya dhambi” Ebr. 5:1.  Mklero anategemewa na  Mungu, Mama Kanisa, waamini na watu wote,  awajibike na yale yote aliyoahidi  kama alivyotamka alipopewa daraja la Upadre. Kwamba alitoka kwenye familia tajiri au maskini, wasomi au wasio wasomi,  katoka kaskazini au mashariki, ukoo huu au ule: yote hayo yanasawazishwa  na wito wa kufanya kazi katika shamba la Bwana kwa ushirikiano na wafanyakazi wenzake. Tangu mwanzo Yesu  aliwateua  “watu kumi na wawili ambao aliwaita mitume, wakae naye, awatume kuhubiri na wawe na uwezo wa kuwafukuza pepo” Mk. 3: 14.  Kwa kutekeleza kwa ushirikiano yale yampasayo, mklero huwa kiungo hai cha kutegemewa na chenye heshima cha mwili wa Kristo.  Taifa la Mungu linahitaji maklero wanaotoa huduma za kiroho ili watu wasiwe kama kondoo wasio na wachungaji kwa kukosa kumjua Mungu.”Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa…Nami nitawapa ninyi wachungaji wanipendezao moyo wangu, watakaowalisha kwa maarifa na fahamu” Hos.4:4 na  Yer.3:15.  Waamini wana haki kupata huduma za kichungaji kwa sababu wanao wachungaji.  Waamini wanatambua kwa kuona na kulinganisha hali zao zinavyohangaikiwa na wachungaji wao.  Waamini ni watu wa Mungu na maklero ni wahudumu muhimu wa watu wa Mungu. Heshima ya mhudumu ipo kwenye uangalifu na uaminifu wake.  Basi Mungu awe yote katika wote. Mklero akumbuke kuwa Mungu anamwona na watu wanamwona, asijidanganye kwamba haonekani; ajitambue na kujitunza vizuri kiaminifu.

 

b). Mtawa anategemewa atoe ushuhuda wazi kwamba hakugawanyika bali  “hujishughulisha na mambo ya Bwana apate kujitolea mwili na roho kwa Bwana” 1Kor.7:34a.  Maisha ya mtawa yatoe unabii kwamba mwanadamu asivurugike akili akihangaika juu ya chakula na chakunywa bali Injili yamdai awekeze katika Ufalme sasa na mengine yote atapewa kwa ziada. (Lk.12: 29-31).  Ulimwengu unahitaji kuona mifano ya wanaume na wanawake walio na furaha na hali ya kutosheka kwa kumchagua Bwana awe urithi wao.  Basi mtawa atoe ushuhuda wa kuishi Injili kwa kufuatana na viapo vya nadhiri au ahadi zake kwa Mungu, kwa Kanisa na kwa Shirika.  Taifa la Mungu linahitaji watawa wanaojitoa kwa sala, kwa sadaka na kwa kutoa huduma za kuleta mapinduzi ya kiinjili katika maisha ya watu. Vijana na watoto waone ushujaa katika maisha na utume wa watawa. Mtindo wa maisha yao udhihirishe hali ya furaha na kutosheka na wito ili vijana wavutwe kujiunga na maisha ya kitawa.  Ulimwengu uwaheshimu watawa kwa vile wao wenyewe wanajiheshimu, wanaheshimiana, wana heshima na wanaheshimika.

 

c). Mlei ana nafasi na wajibu wa kipekee wa kufikisha mwanga wa Injili katika sekta zote za maisha ya mwanadamu kwa vile anafika kote huko.  Kwa mujibu wa Ubatizo na Kipaimara mwamini Mlei anaambiwa yeye kuwa ni chumvi ya dunia na mwanga wa ulimwengu.  Wajibu wake kama chumvi ni kuhifadhi upendo, kuleta ladha ya upamoja na kuondoa uregevu katika utendaji.  Wajibu wake kama mwanga ni kuondoa giza la uongo, udanganyifu, rushwa na kutetea haki kwa wote hasa kwa wanyonge (Mt. 5:13-16).  Wakristo wa kwanza walizingatia “kujifunza kutoka kwa mitume, kuishi pamoja kindugu, kumega mkate na kusali …wakakishiriki chakula hicho (Ekaristi) kwa furaha na moyo mkunjufu.  Walimtukuza Mungu, wakapendwa na watu wote” Mate.2:42, 46b-47a. Sasa ni zamu yetu. Wale walikuwa wakristo wa kwanza; sisi ni wakristo wa sasa lakini uzi ni ule ule. Hakuna ukristo halisi nje ya ushuhuda wa wakristo waliofuata kwa karibu  lile vuguvugu la Roho Mtakatifu aliyewapa nguvu za kuishi maisha mapya ya Injili kwa ujasiri na udumifu katika imani licha ya madhulumu mengi;”Mungu Baba aliwateua nyinyi kufuatana na kusudi lake, na mmefanywa watakatifu na Roho mpate kumtii Yesu Kristo na kusafishwa kwa damu yake” 1Pet. 1:2  Maisha adilifu katika ujana, ndoa, urafiki, familia, JNNK, kazini, kwenye burudani na katika matatizo ndiyo nafasi maalum ya kumtambulisha mkristo anayejali kuzingatia nafasi yake katika mpango wa Mungu.

 

                                        DIRA  YETU.

 

7.KAULI MBIU:  Kutokana na maelezo ya hizo alama kwenye nembo,  maneno yatakayoeleza azma ya awamu hii ni:  KUWAJIBIKA NA KUSHIRIKIANA KATIKA  KRISTO.  Mtume Paulo anaeleza uhai wetu wa imani akitumia mfano wa mwili mmoja ulio katika ushirikiano wa viungo vingi. “Lakini kama ilivyo, Mungu alizipanga sehemu hizo tofauti katika mwili kama alivyopenda.  Kama sehemu zote zingekuwa kiungo kimoja, mwili ungekuwa wapi?  Ukweli ni kwamba, sehemu za mwili ni nyingi, lakini mwili ni mmoja…ili kusiweko na utengano katika mwili, bali viungo vyote vishughulikiane.  Kama kiungo kimoja kinaumia viungo vyote huumia pamoja nacho.  Kiungo kimoja kikisifiwa viungo vingine vyote hufurahi pamoja nacho.  Basi, nyinyi nyote ni mwili wa Kristo; kila mmoja wenu ni kiungo cha mwili huo” 1Kor. 12: 18-20, 25-27.  Kauli mbiu hii inaweka changamoto kwa kila mwamini  ajitafakari anavyokuwa kiungo hai cha mwili  wa Kristo yaani Kanisa.  Uhai wa mwamini ni kule kuona fahari katika Ukombozi unaopatikana kwa njia ya Msalaba wa Bwana, kuzingatia kwa makini neno la Mungu na mafundisho ya Kanisa, kushiriki sakramenti hasa Kitubio na Ekaristi ili awe katika mwungano hai wa neema, na kushirikiana na waamini wengine katika maisha ya pamoja kwenye familia, jamii, mashirika na vyama  vya kitume, bila kusahau jumuiya ndogo ndogo za kikristo.

 

Yesu mwenyewe anahimiza kuwajibika kama alama hai ya kuhusiana naye: “Maana yeyote anayefanya atakavyo Baba yangu aliye mbinguni, huyo ndiye ndugu yangu, dada yangu na mama yangu” Mt.12:50.  Tena , “Si kila aniambiaye, ‘Bwana, Bwana’, ataingia katika ufalme wa mbinguni; ila ni yule tu anayetimiza matakwa ya Baba yangu aliye mbinguni” Mt. 7:21.  Zaidi ya hayo, uwajibikaji wa Mungu wadhihirishwa na uumbaji, hifadhi na uendelezaji wa uhai katika viumbe vyote. Sira 16: 26-30.  Uwajibikaji wa Mkombozi wetu ndio wokovu wetu: “Chakula changu ni kufanya anachotaka yule aliyenituma na kuitimiza kazi yake…Nia yangu si kufanya nipendavyo mwenyewe, bali apendavyo yule aliyenituma”  Yoh. 4:34 na 5:30c.  Sisi wafuasi wa Yesu hatuna budi kufuata mfano na maagizo ya Mwalimu wetu.  Yeye aliwajibika na kushirikiana na Baba na Roho Mtakatifu na wanadamu.  Alituombea uwajibikaji na ushirikiano katika sala maalum kwa wanafunzi wake: “Waweke wakfu katika ukweli; neno lako ni ukweli.  Kama vile ulivyonituma ulimwenguni, nami pia nimewatuma wao ulimwenguni; na kwa ajili yao mimi mwenyewe najiweka wakfu ili nao pia wafanywe wakfu katika ukweli…Naomba ili wote wawe kitu kimoja.  Baba! Naomba wawe ndani yetu kama vile wewe ulivyo ndani yangu nami ndani yako.  Naomba wawe kitu kimoja kusudi ulimwengu upate kuamini kwamba wewe ulinituma.  Mimi nimewapa utukufu uleule ulionipa mimi, ili wawe kitu kimoja kama nasi tulivyo mmoja; mimi niwe ndani yao, nawe uwe ndani yangu; naomba wakamilishwe na kuwa kitu kimoja, ili ulimwengu upate kujua kwamba wewe ulinituma, na kwamba unawapenda wao kama unavyonipenda mimi” Yoh. 17: 17-19, 21-23.  Anayotuombea Yesu ni umoja utakaopatikana kwa njia ya kila kiungo kuwajibika kikamilifu kwa manufaa na usitawi wa mwili mzima yaani Kanisa.  Kwa hiyo kila mwamini anakabiliwa na changamoto mbili: ya kuwa hai sio hoi; na kushirikiana na waamini wengine ili Kristo awe Alfa na Omega katika yote.

NAMNA BORA YA KULEA IMANI NI KUWA NA MSIMAMO MMOJA JIMBONI.

 

                   TARATIBU  ZA  HUDUMA  ZA  SAKRAMENTI  JIMBONI  MOSHI.

 

“Kwa namna hiyo ametujalia zawadi kuu na za thamani ambazo alituahidia, ili kwa zawadi hizo mpate kuziepa kabisa tamaa mbaya zilizomo duniani, na kuishiriki hali yake ya kimungu” 2Pet.1:4.

 

I.                    UBATIZO:

 

1.                    WATOTO  WACHANGA

i.                         Mara mtoto azaliwapo fomu ichukuliwe ofisini ikajazwe jumuiyani.

ii.                       Baada ya kujazwa vizuri katika JNNK fomu ipelekwe kwa Padri mlezi kwa maelekezo muhimu juu ya semina na ubatizo.  Kila JNNK iwe na muhuri na utumike kuidhinisha mambo ya JNNK.

iii.                      Wazazi na msimamizi wa ubatizo wahudhurie semina ya uwajibikaji na ushuhuda wa imani kwa siku moja kabla ya ubatizo.  Kubatiza ni kumzaa mtoto kiroho!

iv.                     Ubatizo wa wachanga ufanyike siku mwafaka ambayo wazazi wote wawili (kama wapo) wataweza kuhudhuria ibada.

 

2.                    WATU  WAZIMA.

 

i.                         Wajiandikishe ofisini kwa ajili ya mafundisho ya dini na Biblia.

ii.                       Wahudhurie mafundisho mpaka wayajue na kushinda mitihani pamoja na kulipa ada.

iii.                      Wajaze fomu za kuomba ubatizo kupitia JNNK zao na kuzipeleka fomu kwa Padri kiongozi wa mafundisho ya dini.

iv.                     Watu wazima hupata Sakramenti za awali yaani Ubatizo, Kipaimara na Ekaristi, zote kwa wakati mmoja.

v.                       Wakristo wasio wakatoliki hupewa mafundisho ya katekisimu na kupokelewa rasmi kwenye ukatoliki kwa ibada maalum.  Kushirikiana na wakatoliki kwenye ibada na JNNK haitoshi kumwingiza mtu kwenye imani Katoliki!  Jambo hili lisifanywe kwa kulipua na haraka.

 

II.                              EKARISTI  TAKATIFU  AU  KOMUNYO  YA  KWANZA:

 

1.              WANAFUNZI – SHULE  YA  MSINGI.

i.         Wanafunzi wa darasa IV na la V wenye kufahamu sala waandikishwe katika JNNK        

                    kwa kulipa ada itakayotumika kuwaandalia mitihani ya kuandika.  Watafundishwa                             

                    kwa mwaka mmoja na kila mmoja awe na katekisimu ya mafundisho.

        ii.        Wahudhurie mafundisho kiaminifu na washinde mitihani kwa kupata alama 50-100.                                                                              

                    Padri asimamie kwa makini zoezi lote la maandalizi.

iii.                    Waboreshe tabia zao ziendane na mafundisho waliyopewa.  Wazazi na wasimamizi 

wa ubatizo pamoja na viongozi wa JNNK wasimamie malezi kwa ushirikiano.

iv.                   Walioshinda mitihani waungame vizuri na walipe ada kama watakavyoelekezwa.

v.                     Wanafunzi watapokea Komunyo ya kwanza tarehe watakayopangiwa na Paroko.

 

III         KIPAIMARA:

 

              WANAFUNZI – SHULE YA  MSINGI.

i.                     Wanafunzi darasa la V na la VI waliokwishapokea Ekaristi waandikishwe katika

JNNK kwa kulipa ada kwa ajili ya mitihani.  Wataffundishwa kwa mwaka mmoja na kila mmoja awe na Katekisimu ya Biblia na Biblia (Ziko Bookshop).

ii.                   Wahudhurie mafundisho kiaminifu, wakomae kitabia na washinde mitihani kwa

Kupata alama 50-100.  Padri na mkatekista mhusika wasimamie maandalizi yote

iii.                  Mafundisho yawawezeshe kukomaa kimaadili, yawape kionjo cha imani ya

matendo ya kweli. 

iv.                 Walioshinda mtihani waungame vizuri na kulipa ada watakavyoelekezwa.

v.                   Wanafunzi watapokea Kipaimara tarehe watakayopangiwa na Paroko.

vi.                 Wasimamizi wa Ubatizo wasishinikizwe kugharamia sherehe za maadhimisho.

 

2.              WANAFUNZI --  SEKONDARI NA VYUO:

i.                       Wanafunzi waanze mafundisho ya Katekisimu mara wafunguapo shule.

Wajizoeshe Biblia na kuhamasishwa kuwa na KKK ufupisho makini.

ii.                     Majina ya hao wanaoandaliwa mashuleni yafikishwe ofisini na vyeti vyao vya

             ubatizo viwe tayari kwa mwalimu mlezi mwezi Juni.

iii.                    Watafanya mtihani mwanzo wa mwezi Septemba na watalipia mtihani huo. Padri

              mlezi wa parokiani  ahusike na utaratibu huu.

iv.                   Watakaoshinda watalipa ada ya sakramenti na kuwasilisha vyeti vya Ubatizo.

v.                     Wanafunzi wa Sekondari na Vyuo watapokea Kipaimara Septemba baada ya kupokea sakramenti ya Kitubio(wachache hupokea Ubatizo na Ekaristi siku chache kabla ya Kipaimara kutegemea na maandalizi waliyopewa).

 

        IV         SAKRAMENTI  YA  KITUBIO (UPATANISHO).

 

i.                      Kila mkristo apokee Sakramenti hii ili awe katika hali ya neema.

ii.                     Maungamo yapangiwe utaratibu unaoeleweka kwa waamini na ufuatwe.

 

 

 

 

 

V.                  SAKRAMENTI  YA  NDOA.

 

i.                       Wachumba wakiwa na vyeti vya ubatizo wasindikizwe ofisini na kiongozi JNNK

              ili wakaandikishe ndoa.  Wawe na kibali cha wazazi wa pande zote mbili.

ii.                     Wakati ndoa ikitangazwa, mafundisho ya Kanisa juu ya sakramenti ndoa na majukumu yake yatolewe kwa dhati, kwa muda wa kutosha na kwa siku maalum.

iii.                    Yafaa wachumba wapate vitabu vya kuimarisha imani na mahusiano yao k.v. Biblia, Njia yetu katika Mapendo na Ndoa na KKK ufupisho makini n.k.

iv.                   Ndoa yaweza kufungwa wakati wa kufaa maarusi wakisha maliza mafundisho yao na kulipa Shahada ya Ndoa(Amri ya Serikali ikikiukwa ni kosa la jinai).

v.                     Maarusi na wapambe wavae mavazi ya heshima na ya kiibada, tena wawepo kiroho katika ibada wakiombea udumifu na usitawi wa ndoa hiyo.     

 

VI.                 SAKRAMENTI  YA  WAGONJWA.

 

   i         Mwanafamilia apelike taarifa kwa kiongozi JNNK kuhusu hali ya mgonjwa na

             sakramenti anayohitaji.

   ii.        Kiongozi JNNK amwendee Padri mlezi kuhusu hitaji la mgonjwa ili taratibu za

              huduma zipangwe.

iii.                    Padri mlezi anaweza kupanga na uongozi JNNK Mtaa/ Kanda namna ya

              kuwafikia wagonjwa muda wowote lakini hasa wakati wa Pasaka.

iv.                    Wagonjwa wasicheleweshwe kupelekwa hospitali.

v.                     Meza yenye kitambaa safi na mshumaa iandaliwe nyumbani kwa ajili ya       kuadhimishia Sakramenti ya Wagonjwa.

 

VII:        WANAOPENDA  KUWA  MAPADRE  NA  WATAWA:

 

    i.          Mwenye kusikia msukumo wa kuwa Padri au Bradha au Sista amwone Padri

                mlezi wa JNNK ili aelekezwe taratibu za kufuatilia wito wake.  Inafaa sana

                watoto na vijana wajiunge na Mashirika ya Utoto wa Yesu, Lejio, Bikira Maria,

                Mt. Aloisi, TYCS na VIWAJIMO ili wapate humo malezi endelevu.

            ii.          Baba na Mama familia wawe makini kuilea miito ya Mungu na Kanisa katika

      mazingira ya upendo wa kiristo yaani sala, kuthaminiana na ushirikiano ndani ya

      familia yao badala ya kuwaachia walezi wengine jukumu hilo.

 

VIII                    MAZIKO.

 

    i.           Kifo cha mkristo kikitokea ripoti ifikishwe mapema kwa Padri mlezi wa JNNK.                                 

                 Daftari ya mahudhurio jumuiyani ipelekwe ofisini ili iwasaidie Padri mlezi,

                 Kiongozi JNNK na Mwanafamilia kupanga taratibu za maziko.

    ii.          Endapo Padri hataweza kuadhimisha ibada ya maziko, amwandae Mhudumu

                 Mlei (Mkatekista) kutoa huduma hiyo.

   iii.          Ikiwa mkristo amefariki nje ya eneo anamoishi na kufahamika, barua ya Padre  

                 aliyemhudumia kiroho itahitajika kueleza kama anastahili maziko ya kikristo.

    iv.         Ikumbukwe kwamba maziko ya kikristo ni heshima apewayo mkristo aliyeishi

                  imani pamoja na waamini wenzake.  Maziko sio Sakramenti.

   

 

 

 

 

 

 

 

         

HITIMISHO.

 

Kazi kubwa kwetu sasa ni kupata MALEZI YA FIKRA, DHAMIRA NA MOYO ILI TUWEZE KUTEMBEA PAMOJA.  Twahitaji Semina za stadi za maisha ya kijamii na ya kiroho, mafungo, warsha, maigizo na hasa kupanga malezi endelevu kwa vikundi mbalimbali kama Mapadri, watawa, walimu, vijana,wanandoa na mashirika ya kitume.  Tunazo changamoto za kibinafsi, kifamilia,kijumuiya, kijamii, kijimbo, kitaifa na kimataifa.  Tunao uwezo wa  kutumia vitendea kazi tulivyo navyo kama Biblia, Diocesan Directory, Katiba za vyama na mashirika ya kitume, Katiba ya Halmashauri ya Walei, Katekisimu ya Kanisa Katoliki-Ufupisho makini,  Kitabu cha JNNK cha Padri L.Massawe na vitabu vingine vya kukuza ufahamu wa kutekeleza tunu za Injili katika maisha ya binafsi na ya pamoja.  Biblia na Katekisimu ni hazina bora sana za kujenga waamini na kuwawezesha kuzima mashambulizi ya wazushi na wapotoshaji.  Tuweke nguvu pamoja tuishi maisha tele ya imani kwani Mungu ametutoa mbali.  Malezi yafungue mioyo na akili zetu tuweze kutembea pamoja na Yesu aliye Njia, na Ukweli na Uzima. 

Pamoja na malezi, tunapaswa kuchukua hatua za makusudi tuwe na mawasiliano sahihi na  ya ukaribu zaidi.  Watu wanaoishi pamoja wazungumze na kupanga mambo kwa pamoja.  Viongozi bora hushirikisha wanaoongozwa ili nao washirikishe mawazo yao.  Kwa kuthaminiana tutatajirishana sana.  Wakati umefika wa kuambiana ukweli na kuishi ukweli ili tuweze kuwa na amani na Mungu na wenzetu na hata na nafsi zetu sisi wenyewe.   Mpango wa Mungu “ni kukusanya pamoja viumbe vyote chini ya Kristo” (Ef. 1: 10)  Je!  Wewe  uko tayari na unapenda kushika sehemu yako katika mambo yale Mungu aliyokuwekea katika ufalme wa mwanga? (Kol.1:12).

 KARIBU  BASI  TUWAJIBIKE  NA  TUSHIRIKIANE  KATIKA  KRISTO.

 

           Imetolewa Sikukuu ya Pentekoste

                  Mei 11, 2008

                         + Isaac Amani.

                          Askofu Jimbo Moshi.

 

 

 

 

Haki zote zimehifadhiwa. 

(Back)

 
P.O Box 3041 Moshi, Tanzania.   Tel. +255-27-2752157 [Chancery], +255-27-2752089 
Fax: 0255-27-2750934.[Bishop's House]
Web.  www.moshidioces.org  Email; bishopshouse_moshi@yahoo.co.uk
This site is hosted by CatholicWeb.com | TheCatholicDirectory.com
Powered by CompBiz EZWeb© software.
Server management powered by Spiderhost.